Wanachama wa upinzani FDC Uganda washtakiwa kwa ugaidi
HABARI
Published on 30/07/2024

Wafuasi 36 wa chama cha upinzani cha FDC nchini Uganda wamefikishwa mahakamani mjini Kampala wakikabiliwa na mashtaka ya ugaidi.

FDC ni miongoni mwa vyama vikubwa vya kisiasa nchini Uganda kinachoongozwa na Dkt Kizza Besigye, mwanasiasa mkonwe wa upinzani nchini humo ambaye amewahi kugombea urais mara nne.

Wakili wao, Erias Lukwago, amewaambia waandishi wa habari nje ya mahakama  mjini Kampala kwamba watu hao walikamatwa nchi jirani ya Kenya katika mji wa Kisumu, walikokuwa wamekwenda kushiriki warsha kuhusu  uongozi na kwamba mashtaka yanayowakabili wateja wake hayana msingi.

Kulingana na taarifa za mashtaka watu hao walikwenda kupata mafunzo ya kigaidi na kwa kuwa hawakuwa na mwenyeji rasmi nchini Kenya, polisi ya Kenya iliwasiliana na vyombo vya usalama vya Uganda kabla ya kuwakamata na kisha kusafirishwa  nchini Uganda.

Dkt Kizza Besigye ameikosoa hatua hiyo ya kukamatwa wafuasi wa chama chake  na kuulaumu utawala wa Kenya kwa kufanya hila.

Wafuasi hao 36 wa FDC wakiwemo wanawake watatu wamepelekwa rumande hadi tarehe 13 mwezi Agosti.

Comments
Comment sent successfully!